Friday 24 April 2015

LORENZO

Lorenzo: Che meingia, usiku achekelewa

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Kwa miale yake mawingu azikata

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Na kutawanya giza aliyezagaa

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Kama mayungi majini yanavyolewa

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Jua laoneka wazi. Litazunguka

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Falaki yake likiangaza mimea.

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Lilo jicho lake Mungu huchemsha anga

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Hapa bustani lazima nipande tuka


&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Mama ardhi ni mwenye miujiza kweli.

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Mji mwake ndimo tukifa huzikwa sisi

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Na huzalishwa dhuria mwake tumboni

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Ambao huwa mlo aina anuwai

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Kwa viumbe vyote vilio na uhai.

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Alamina kujaza dunia arzaki

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Majaza yasiyokuwa nacho kifani

&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp&nbsp Alhasili: miti, mawe nazo madini


&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Yote chimbuko yao ni ardhini hapa

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Walakini shida huwa yeye ingawa

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Huzingatia kuleta yaliyo mema.

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Wengine nao huyatumia vibaya.

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Ila, isipokuwa kwa nahusi. Badala

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Insafu nuiwa. Patukia ukuba

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Usio wa kutazamiwa. Mfano mmoja

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Ni hili ua: Ni sumu tena ni dawa.


&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Ukililamba unakufa wako mwili

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Kilinusa, unachechemka wote mwili.

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Zimefanywa zote hizo mardufu kazi

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Kwa kutumiwa kitu kimoja tu hiki.

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Hivyo hata binadamu tulivyo nafsi

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Tuna hisani pamoja na uhasidi

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Maulana basi ubaya yetu ndani

&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160&#160 Sije tawala juu yake hasanati.

Wednesday 7 January 2015

TANZU TATU ZA FASIHI


Hakika hamna tanzu ya fasihi iliyo bora kuliko nyingine. Kama vile jazanda ya mti ilivyoonyesha. Tanzu zote tatu zinatoshana barabara kwa hadhi ya kuakilisha fasihi. Iwe

(i) Andishi (matawi): inayokumbatia riwaya, tamthilia na diwani;

(ii) Simulizi (majani): inayokumbatia tamba, kukariri, kuimba na mijadala; au

(iii) Onyeshi (maua): inayokumbatia uigizaji, tamasha kama vile denzi na mieleka na sinema.

Tunapotaka kutathmini ubora wa fasihi vipo vigezo vinavyotumika ambavyo hutangulia na kutofautisha fasihi katika sehemu mbili maarufu: (a) fasihi dhati na (b) fasihi pendwa

Saturday 8 February 2014

THESUSE NA JITU MINOTA



Thesuse na mama yake, Athera, waliishi chini ya mlima mkubwa mahali palipoitwa Trozeni. Thesuse alipokuwa angali mchanga baba yake, Egesu, aliinua jiwe kubwa lililokuwa mlimani katikati ya msitu na hapo alilaza upanga na sapatu chini yake. kisha akamuambia Athera kuwa Thesuse atakapokuwa mkubwa na mwenye nguvu za kuinua jiwe hilo basi amfuate kule Atheni –huko Egesu alikuwa mfalme wa Attika.


Thesuse alipokuwa mkubwa, aliweza kuchomoa ule upanga na sapatu kutoka chini ya jiwe na akafunga safari kuelekea Atheni. Safari ya kuelekea Atheni haikuwa rahisi, ilikuwa na misitu mengi na nyuma ya mawe makubwa walijificha majitu na majambazi. Lakini, Thesuse alimuaga mama yake na kujaribu bahati yake. Hata hakuwa ameenda mbali sana alipovamiwa na Perifite –aliyejulikana kwa utani kama “mbeba rungu.”  Alionekana jamaa wa kutisha sana akiwa na amebeba hiyo runga yake kubwa ya chuma. lakini Thesuse alimkabili na muda si mrefu alikuwa amemwangamiza hapo barabarani. Akachukua hata hiyo rungu yakena kuendelea na safari.


Mbele zaidi alikutana na Sinusi “mkunja miti.” Ukatili wake ulikuwa wa kuwararua wasafiri kwa kuzinyambua miti mbili kubwa na kisha kufunga msafiri kwa miti hizo na kuziwachilia zinepuke na kumrarua mtega nyara huyo. Sinusi mwenyewe alikuwa pia na runga lakini haikuwa na nguvu kama ile Thesuse alikuwa amebeba. basi siku hiyo ilikuwa Sinusi aliyeraruliwa na miti hizo zenye mnaso. Akiendelea na safari alikutana na jambazi aliyeitwa Sironi ambaye alilazimisha wasafiri wamwoshe mikuu hatimaye aliwapiga teke na kuwaangusha kutoka ngomeni hadi baharini. lakini wakati huu ilikuwa Sironi aliyepokea adhabu hiyo. Mbele kidogo paliishi jambazi mwingine kwa jina Porokruste ambaye alijifanya kuwa mtu mkarimu na kuwakaribisha wageni kwenye chumba chake lakini, wakipatikana kuwa  warefu kuliko kitanda chake, aliwakata vichwa au mikuu hadi watoshee. Na, wakiwa wafupi, aliwavuta shingo na miguu hadi waliporefuka na kutoshea kitanda hicho. lakini pia Porokruste alipata adhabu yake kama tu wale majambazi na majitu waliyomtangulia kwenye hii safari ya kuelekea Atheni.


Wakati huo mrembo Medai ambaye pia alikuwa mlozi mkubwa alikuwa akiishi kwenye ikulu ya mfalme. Alikuwa na mtoto kijana aliyemtarajia kumridhi mfalme Egesu kwa hivyo alimtengenezea Thesuse kinywaji kilichojaa sumu na kumwandalia kwenye kikombe kikubwa. Alimwambia mfalme kwamba mgeni huyo wake alikuwa mkora ambaye alikuwa amekuja tu kumpokonya ufalme wake na hivyo akamshawishi mfalme ampe Thesuse kinywaji hicho. Thesuse hakujua njama hiyo na alikuwa ameshainua kikombe ili akunywe kinywaji wakati Egesu alipoona ule upanga wake pamoja na sapatu na akakumbuka mwanawe. Aliruka na kukichukua kikombe hicho chenye kinywaji hatari, na akakitupa mbali.

Medai alitumia mbinu zake na akafaulu kujiponya na kutoroka. kwanza allita uchusichusi kutoka mtoni ukamfunika. Kisha akaiita majitu yake yaliokuwa na mabawa na akaruka kwa gari ambalo majitu hayo yaliivuruta na akatoroka Atheni- asirudi tena. Watu nao hawakuchelewa kumweleza mfalme sifa zote za ujasiri wa Thesuse ambazo alizionyesha katika safari yake kutoka Trozeni hadi kifika kwake Atheni. Egesu alifurahia sana ngano hizo hata akatangaza siku tatu za kusherekea kuwasili kwa Thesuse. Lakini kwenye hiyo harakati, alikuja mjumbe mmoja kutangaza kwamba wale wawia kutoka Krete wamewasili.


Ilitokea kwamba hapo zamani, mwana na mridhi wa mfalme Minoso wa Krete aliuawa na Waatheni. Na kulipiza kitendo hicho, mfalme Minoso aliwashambulia Waatheni kwa kikosi chake kikubwa cha jeshi na kuwalazimu Waatheni kukubali masharti yake ambayo yalikuwa kwamba kila baada ya miaka tisa watampa ‘watoto wa kafara’ ambao walikuwa wanaume saba na mabinti saba. Naye aliwachukua hao ‘watoto wa kafara’ na kuwatupa kwa jitu moja kubwa liloitwa Minota ambalo ingawa kiwiliwili chake kilikuwa cha mtu, kichwa chake kilikuwa cha fahali. Minota aliishi pangoni huko Krete Karibu na ikulu ya mfalme. Pango hilo lake lilikuwa na njia nyingi ambazo zilimchanganya yeyote aliengia humo. Hakuna hata mtu mmoja aliyefaulu kurejea kutoka humo pangoni mara tu alipoingia.


Thesuse aliamua kwamba ataangamiza jitu hilo na kukomesha dhuluma hiyo duni ya kuwaua watu kumi na wane wasio na hatia kila baada ya miaka tisa. Na basi, hata kabla ya kuchaguliwa wale vijana ambao wangepelekwa Krete, Thesuse alijitolea muhanga na wale wengine wakachaguliwa kwa kupigiwa kura kama ilivyokuwa desturi. Jambo hilo la Thesuse kujitolea kivyake lilimletea umaarufu sana mbele za watu. Muda si muda, merikebu iliyowabeba watoto hao wa kafara ilinoa nang’a huku imevikwa tanga ya rangi nyeusi kama ilvyokuwa kawaida ila wakati huu mfalme Egesu alimpa mwanawe tanga ingine nyeupe ili aipeperushe kwa merikebu kama atakuwa bado hai wakati wa kurejea.
Walipowasili Krete Thesuse hakuchelewa kumweleza mfalme Minoso kwamba nia yake ilikuwa Kumuua jitu Minota. Minoso alikubali ombi la Thesuse kwamba akifaulu basi yeye na wale wanakafara wengine wataachiliwa huru na tena deni lake litakuwa limelipwa milele. Hata hivyo, Minoso aliongeza sharti kwamba Thesuse ataingia mle pangoni bila upanga wake kuenda kukabiliana na jitu. 


Hapo kwa dari ya chumba ambacho walikuwa wamefungiwa Thesuse na wenzake palikuwa chumba cha binti zake mfalme Minoso, Ariadin na Faidera ambao waliamua kumsaidia Thesuse katika juhudi zake. Walifungulia Thesuse mlango kama wale wengine bado wamelala na kumpeleka hadi palipokuwa hiyo pango maarufu lenye kuta za marumaru zilizong’a kwenye mwangaza wa mwezi. Ariadin alimfichulia “Wakati huu ndiyo mzuri wa kuua jitu hilo kama lingali linalala. Usiongojee hadi asubuhi likishaamka” Ariadin aling’ong’oza. “Maskani yake ni humu katikati mwa pango hili lenye njia nyingi zenye mikato aina ya labiranthi. Fuata sauti ya mg’oroto wake. Pia chukua upanga huu na kipira cha uzi ambao utatumia kupata njia ya kurejelea kutoka pangoni” Kwa hayo maneno, ariadin alibaki kama ameushika mwanzo wa uzi na Thesuse akaingia na mradi wenyewe akiachilia polepole kwa kuelekea ndani, upanga nao thabiti mkononi.


Mle ndani njia zilikuwa kabibu na nyingi zilikuwa na wa mkingo wa gafla bila kuelekea popote na hapo Thesuse ilimbidi arudi nyuma na kutafuta tena. Inasemekana kuwa hapajawai kuwa na mikato za labirathi zilizokuwa za kutatiza kama hizi zilizotengenezwa na mhandisi Dadesulu. Ingia ndani, toka tena; ingia Thesuse aliendelea. Alizidi kusikia sauti ya kung’orota kwa Minota ikiongezeka na kujua kwamba anakaribia makao yake. Kwa hayo yote Ariadin na Faidera waliongojea langoni, Ariadin akishikilia upande wake wa uzi kwa ustadi. Mara walisikia mtetemeko mkubwa na yowe kwa mbali kisha kukawa na kimya kikuu. Ariadin hangeweza kujua kama Thesuse ameuawa au kama hata bado alikuwa na ule mradi ulioviringishwa uzi lakini alianza kuhisi uzi ukivutuavutua halafu muda si mrefu mwana wa mfalme Egesu akajitokeza.


Ile meli iliyowaleta Thesuse na wenzake Krete ilikuwa bado pale ufuoni. Vijana walikuwa wangali wanalala walipoamshwa na mara moja walikuwa safarini kurudi Atheni. Nao pia Ariadin na Faidera kwa kuhofia hasira ya baba yao, waliwafuata. Katika safari hiyo walitua kwenye kisima cha Nakso na wakatengeneza kambi hapo kwa miamba usiku. Kesho yake asubuhi na mapema waliendelea na safari hiyo yao lakini Ariadin alibakia kama amelala na kwa hivyo aliwachwa nyuma. Thesuse hakusahau tu Ariadin ila pia kupeperusha ile tanga nyeupe baba yake alikuwa amempa. Kwa hivyo meli yao ilipojitokeza Atheni na tanga nyeusi juu yake mfalme Egesu alijitupa baharani akidhani kuwa mwanawe hakufaulu.


 * Ariadin alichukuliwa na Bachisu akampeleka angani na kumvisha taji iliyo na nyota tisa kichwani. Yeye huonekana hadi leo angani ya kaskazini.

Sunday 11 December 2011

TABARUKU: BURIANI KWA SAMUEL MUSHI

Mwaka huu umekuwa na hasara zake. Juu ya kutupokonya Profesa Maathai hapa Kenya, umetunyanganya mwana-lugha mkuu na mkongwe ambaye kuaga kwake bila shaka ni hasara kubwa kwa jumuia na wazalendo wa Kiswahili na hasa fani ya fasihi. Tarehe 23 Julai mwakani, mwalimu Samuel Mushi alipiga dunia teke na akaenda zake mbinguni. Alifariki alipokuwa akipokea matibabu katika hospitali mmoja inayofahamika kama Muhimbili National Hospital huko Tanzania. Alikuwa na miaka sabini na miwili (alizaliwa 1939). Hata hivyo, jambo la muhimu ni kuwa alifanya mchango wake na sasa waliobaki nao wafanye yao.
Wengi labda hawamfahamu mwalimu Mushi kwa jina, hasa hapa Kenya, lakini wengi wameshasikia hadithi ya mfalme Edipode ambayo mwalimu huyu aliitafsiri mnamo mwaka wa 1971. Hadithi hiyo, baada ya kutafsiriwa na mwalimu Mushi, ilivuma sana na kuwafikia watu wengi ambao hawangepata fursa ya kuisikia kwa vile wangetatizwa kuielewa katika hati za lugha za kimombo. Ufanisi huo ulikuwa hakikisho tosha kwamba fasihi haina mipaka na hamu ya wanadamu wote kusimuliwa hadithi nzuri ipo. Pia hadithi yoyote ile yawezafikia kila mtu, bora mbinu za kuieneza na kueleza ziwe mwafaka.
Hadithi bila shaka ilikuwa ya Sophocles ambaye tunamwita Sofokile, ila mwalimu Mushi aliipa msisimko wa Kiswahili hata kuifanya ionekana ngano ya hapa nyumbani na wala si ya ughaibuni. Lakini, hiyo sio kazi pekee aliyoifanya mwalimu huyu. Hata kabla ya kuswahilisha Sophocles, alikuwa ameshaswahilisha William Shakespeare -mchezo wa Makbeth akiwa na umri wa miaka 29 tu, na Tufani mwaka mmoja baadaye (1969). Hata hivyo tamthilia hizo hazikufana sana Kenya kwa kufuatia maudhui yao ambao yalilenga sana ushirikina. Kazi hizo alizifanya labda akifuata katika nyayo za mtangulizi wake -Mwalimu Nyerere, ambaye alikuwa amekwishaswahilisha Juliasi Kaizari (1963).
Katika ustadi wa utafsiri fasihi huenda Mushi alimpiku mwalimu Nyerere. Sababu ya kunawiri kwa Mushi kushinda Nyerere (kwa mtazamo wangu) ni kwamba huyu wa pili aliegemea sana fasihi ilihali huyo wa awali aliegemea sana siasa. Mushi alitafsiri akiwa na nia na kutumbuiza na kuongozwa na uhondo wa fasihi, yaani aliwasilisha pamoja na kuwakilisha. Mwalimu Nyerere naye alitamani sana kuangazia maswala ya kisiasa yaliyomo kwenye maandiko husika. Ndipo hata katika tafsiri yake ya "Things Fall Apart" mwalimu Nyerere aliipa mtazamo wa "Shujaa Okonkwo" badala ya "Dunia Imepasuka." Nyerere aliendelea kumwona Okonkwo kama shujaa, ingawa fasili inamtambua kama mtu hafifu.
Ni bayana pia Mushi alichagua hadithi zenye rutuba kubwa ya kifasihi kushinda wengi waliomtangulia. Ingawa hivyo si kusema kuwa hapawezijitokeza mwandishi mwingine akazisimulia kazi hizo na zinginezo kwa ubora kumshinda. Hata mwenyewe alikiri katika utangulizi wa Tufani kwamba "...napenda kusema kama ikiwa upungufu wa tafsiri yangu utauudhi baadhi ya wasomaji kiasi cha kuamsha cheche za shauku ya kutoa tafsiri nzuri zaidi ya mchezo huo au kuifuatisha hadithi ya mchezo huo kwa ukamilifu zaidi...hakuna atakayefurahi kunishinda."
Mchango wa Mushi kwa fasihi haukukomea hapo kwa vile ni yeye aliyekuwa na ujasiri mkubwa kutohoa na kubuni majina mengi ambayo hayakuwepo kabla yake, hasa katika msamiati wa fasihi ya kutafsiriwa. Hakuokopa kumwita Zeus- Zeo, Sophocles- Sofokile, Oedipus- Edipode, na Thebes- Thebe. Msamiati huu unasaidia sana wandishi wa badaye kuandika kwa upesi zaidi bila kusumbuliwa ama kusumbuka kubuni majina mapya kuzungumzia mambo au watu wale wale. Kwa wale ambao wamejaribu kuandika au kuzungumzia fasihi hizo kama Dkt. Richard Wafula (na mimi pia) wanafamu na kufaidi mchango huo wa Mushi kwa makini.
Mushi alipanua mipaka ya utungaji mashairi. Kwa kutafsiri Edipode akitumia mizani sita badala ya nane ama kumi na sita, amekomboa wandishi wengi ambao walikuwa wamefungiwa katika kanuni ambazo wakati mwingine hazitoshelezi tafsiri kikamilifu. Ingawa Stephen Mushi alichangia pia katika uandishi wa mambo mengine kama siasa (vitabu thelathini na moja hivi) lakini, ni kwenye nyanja ya fasihi ambapo nyota yake inang'a na haina mpizani wa dhati. Jinsi tu vile riwaya ya Kusadikika ya Shabaan Robert bado inashikilia upeo kama fasihi bora ya kiasili ndivyo tamthilia ya Mfalme Edipode ya Samuel Stephen Mushi inashikilia nafasi hiyo ya kuwa fasihi- tafsiri bora kufikia leo.
Kumalizia, mimi kama shabiki wa mwenda zake, nimemtugia Mushi shairi lifuatalo

Ulikichukua Kiswahili
Ukakiinua kikawa ni
Lugha ambayo
Ina hadhi ya kimataifa
Ina mengi ya kujivunia
Chombo ambacho
Chawezaelezea chochote
Chaweza kuchambua lolote
Msingi ulio
Imara kueneza fasihi
Bora kuendelezea kazi

Kwaheri mwalimu.
Edwin Musonye
(Edwin Musonye ni shabiki wa fasihi na lugha)
//